Wednesday 22 August 2012

Murabaha (Non- participatory mode) no 1

Wasomi na wachumi wa kiIslam wanapendelea benki za kiIslam zitoe huduma kwa kutumia mifumo shirikishi ambayo ktk moja ya sifa zake kuu ni mteja kushirikiana na benki ktk faida na hasara. Ingawaje, kiufundi mifumo inayotumika sana ni ile mifumo isiyokua shirikishi (non-participatory modes), ikiwemo murabaha, Ijara na salam, ktk makala hii tutazungumzia murabaha.

Murabaha ni aina ya biashara ambayo inakubalika ktk sheria ya kiIslam ambapo muuzaji anamtajia mnunuzi thamani aliyonunulia bidhaa na anaongeza faida yake ambapo sana, mnunuzi atalipa thamani ya bidhaa hiyo pamoja na faida waliyokubaliana kidogodogo na kwa muda unaojulikana.

Bank za kiIslam zinatumia murabaha pale benki inaponunua bidhaa fulani kulingana na matakwa ya mteja na ikamuuzia mteja bidhaa hiyo kwa thamani iliyonunulia na kuongeza kiasi cha faida. Kimsingi, mteja anailipa benki kidogodogo ktk muda watakaokubalina kwa sababu kama angekua na uwezo wa kulipa kwa pamoja asingekua na haja ya kununua bidhaa hiyo kwa kutumia benki, ingawaje, kisheria hazuwiliwi kufanya hivyo. Kiwango walichokubaliana hakitakiwi kubadilika, vinginevyo mazingira ya riba yanaweza yakajengeka.

Baadhi ya masharti ya murabaha:

1- Muuzaji wa bidhaa ni lazima awe ni mtu anaeruhusiwa kuuza kisheria, kwa mfano, huwezi kufanya biashara na mtoto mdogo.

2- Muuzaji ni lazima amiliki kisheria kile anachokiuza

3- Kinachouzwa ni lazima kijulikane

4- Bei ya kitu ni lazima iwe maalum na isibadilike, kwa mfano A ametaja shilingi 500 kua ndio bei ya bidhaa fulani atakayo muuzia B kwa muda wa mwezi mmoja, lakin kama ikipita miezi miwili A atamtaka B alipe Shilingi 510. Ktk hali kama hii bei ya bidhaa itakua haina uhakika, na mauziano ya namna hiyo yatakua ni batili.
Na kuna masharti mengine ya murabaha ambayo yatawekwa wazi zaidi ktk makala zinazokuja.

Uhalali wa kupanga bei maalum na muda maalum na maswali yanayoweza kujitokeza.

Wasomi wengi ktk wakati tulionao wanahalalisha kuuza bidhaa kwa bei tofauti ktk kipindi tofauti na wanaliona hilo ni kama mabadiliko ya kiuhalisia yanayotokana na mahitaji ya soko (supply and demand),kwa mfano bidhaa inaweza kuuzwa sokoni kwa Sh 500 leo na bidhaa ileile ikauzwa kwa Sh 510 kesho au ikawa inauzwa kwa bei tofauti wakati uleule ktk soko jingine. Kwahiyo ni halali kwa muuzaji kumuambia mteja kwamba kama utanunua bidhaa hii leo nitakuuzia kwa Sh 500 lakin kesho itauzwa kwa Sh 510. Mabadiliko hayo ya bei yanatakiwa yatokane na hali halisi ya soko na yasionekane kama ni fidia ya wakati. Ktk mazingira kama hayo muuzaji haruhusiwi kutumia hadaa kwa ajili ya kupata bei nzuri.

Tofauti ya murabaha ktk benki za kiIslam na zile zisizokua za kiIslam
Ni vyema tukakumbushana kwamba murabaha inatumiwa sana na benki za kiislam na zisizokua za kiIslam ktk biashara mbalimbali, kwa mfano murabaha unaweza kutumika kwenye viwanda vya muda mfupi, ktk biashara ya nyumba na kununulia mashine za kufanyia kazi. Wakati murabaha hauhusiani na banki za kiIslamu tu, kuna tofauti ya msingi kati ya benki hizo mbili, kwa mfano faida inayopatikana ktk benki za kiIslam haihusiani na kitu kinachojulikana kama (opportunity cost of money).

Tofauti nyingine ni ile inayohusiana na mteja kushindwa kulipa kwa kipindi walichokubaliana na benki. Kwa benki za kiIslam, itategemea kwanini mteja ameshindwa kulipa kwa taimu aliyopangiwa, kwa mfano kama kuna sababu za msingi basi ataongezewa muda, na kama hana sababu za msingi basi anaweza kupigwa faini lakin faini ile haitatumiwa na benki ktk shughuli zake na badala yake itatolewa bure kwa mashirika ya misaada. Maswala haya yatazungumziwa kwa ufafanuzi zaidi baadae.

Kwa kuzingatia mazingira ya kibiashara ktk wakati tulionao, murabaha unahusiana na mikataba mbalimbali kama vile maombi ya mteja kununua bidhaa Fulani, ahadi ya mteja kwamba atainunua hiyo bidhaa, ahadi ya wakala na mkataba wa kuwepo maombi na kukubali kutoka pande zote mbili benki na mteja. Ahadi ya kununua bidhaa kwa mteja kutoka benki ni lazima itekelezwe (binding), kwa maana mteja anatakiwa kisheria atekeleze ahadi yake na kama akivunja ahadi yake baada ya benki kununua bidhaa waliokubaliana, mahakama inaweza kutumika kumlazimisha mteja kutekeleza ahadi yake. Hilo linaweza kufanyika kwa kutumia njia mbili, ima mteja kununua kitu alichoahidi au kulipa gharama zilizotumika ktk swala hilo, lakini hilo la mteja kupigwa faini, halizingatiwi kama ni badali ya (opportunity cost) kwani kufanya hivyo kutajenga mazingira ya riba. Pamoja na mambo mengine benki ili iwe na uhakika na inachokifanya inaruhusiwa kisheria kumlazimisha mteja kununua kitu kinachojulikana kama Hamish jiddiah ambayo ni kiasi fulani cha pesa kitakachotolewa kama deposit ambayo itafahamisha kwamba kweli mteja ana nia ya dhati ya kununua bidhaa kama alivyoahidi

Sheria inasemaje kama mteja akilipa mapema kuliko muda aliopangiwa?

Kwa kawaida kiwango cha faida kilichowekwa ktk murabaha hakibadiliki kwa mteja kulipa mapema, ispokua benki inaweza kuhamasisha wateja wake kulipa mapema na kwahivyo basi wakaahidi wateja wao aina fulani ya zawadi. Ktk mazingira ya kawaida wasomi wa kiislam (scholars) hawaruhusu mtu kulipa mapema kwenye murabaha kwani itakua haina tofauti sana na biashara ya riba ambayo imekatazwa. Accounting and Auditing Organization for Islamic financial Institutions (AAOIFI’s) wanaona kwamba, kama benki haikumuahidi mteja kitu chochote kwa kulipa deni lake haraka, basi benki itakua na hiyari kati ya kutoa zawadi na kukataa. Hayo yalikua ni maelezo ya murabaha kwa mukhtasar. Kwa haya machache tutaishia hapa na kama kutakua na swali lolote basi usisite kuwasiliana nasi. Shukran

No comments:

Post a Comment